Matthew 17:1-13

Yesu Abadilika Sura Mlimani

(Marko 9:2-13; Luka 9:28-36)

1 aSiku sita baada ya jambo hili, Yesu akawachukua Petro, Yakobo na Yohana ndugu yake Yakobo, akawapeleka juu ya mlima mrefu peke yao. 2 bWakiwa huko, Yesu alibadilika sura mbele yao. Uso wake ukangʼaa kama jua na nguo zake zikawa na weupe wa kuumiza macho. 3Ghafula wakawatokea mbele yao Mose na Eliya, wakizungumza na Yesu.

4Ndipo Petro akamwambia Yesu, “Bwana, ni vyema sisi tukae hapa. Ukitaka, nitafanya vibanda vitatu: kimoja chako, kingine cha Mose na kingine cha Eliya.”

5 cPetro alipokuwa angali ananena, ghafula wingu lililongʼaa likawafunika, na sauti ikatoka kwenye hilo wingu ikisema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa. Ninapendezwa naye sana. Msikieni yeye.”

6 dWanafunzi waliposikia haya, wakaanguka chini kifudifudi, wakajawa na hofu. 7 eLakini Yesu akaja na kuwagusa, akawaambia, “Inukeni na wala msiogope.” 8Walipoinua macho yao, hawakumwona mtu mwingine yeyote isipokuwa Yesu.

9 fWalipokuwa wakishuka kutoka mlimani, Yesu akawaagiza, “Msimwambie mtu yeyote mambo mliyoyaona hapa, mpaka Mwana wa Adamu atakapofufuliwa kutoka kwa wafu.”

10 gWale wanafunzi wakamuuliza, “Kwa nini basi walimu wa sheria husema kwamba ni lazima Eliya aje kwanza?”

11 hYesu akawajibu, “Ni kweli, Eliya lazima aje kwanza, naye atatengeneza mambo yote. 12 iLakini nawaambia, Eliya amekwisha kuja, nao hawakumtambua, bali walimtendea kila kitu walichotaka. Vivyo hivyo Mwana wa Adamu pia atateswa mikononi mwao.” 13 jNdipo wale wanafunzi wakaelewa kuwa alikuwa anazungumza nao habari za Yohana Mbatizaji.

Copyright information for SwhNEN